MUNGU NI KIONGOZI WA MAPITO YAKO







Yehova Anawaongoza Watu Wake
“Yehova [atakuongoza] sikuzote.”—ISA. 58:11.
JE, UNAWEZA KUELEZA?
Ni kwa njia gani wanaume waliotumiwa na Mungu kuongoza watu wake wa kale na vilevile Yesu Kristo walionyesha kwamba . . . 
  • walitiwa nguvu na roho takatifu?
  • walisaidiwa na malaika?
  • waliongozwa na Neno la Mungu?
1, 2. (a) Wale wanaoongoza kati ya Mashahidi wa Yehova wanatofautianaje na viongozi wa dini nyingine? (b) Tutachunguza mambo gani katika makala hii na itakayofuata?
“KIONGOZI wenu ni nani?” Mashahidi wa Yehova huulizwa swali hilo mara nyingi. Na hilo halishangazi! Dini nyingi huongozwa na mwanamume au mwanamke mmoja. Tofauti nao, tunafurahi kuwaeleza wanaotuuliza kwamba Kiongozi wetu si mwanadamu asiye mkamilifu. Badala yake, tunafuata mwongozo wa Kristo aliyefufuliwa, ambaye pia hufuata mwongozo wa Baba yake, Yehova.—Mt. 23:10.
2 Hata hivyo, kuna kikundi cha wanaume wanaosimamia kazi kati ya watu wa Mungu leo ambao Biblia huwaita “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Basi, tunajuaje kwamba kwa kweli Yehova ndiye anayetuongoza kupitia Mwana wake asiyeonekana? Katika makala hii na itakayofuata, tutachunguza jinsi ambavyo kwa karne nyingi Yehova aliwatumia wanaume fulani kuongoza watu wake. Makala zote mbili zitaonyesha mambo matatu yanayothibitisha kuwa kwa kweli Yehova ndiye aliyekuwa akiwatumia wanaume hao, na hivyo kuthibitisha kwamba alikuwa na bado ndiye Kiongozi wa watu wake.—Isa. 58:11.
WALITIWA NGUVU NA ROHO TAKATIFU
3. Ni nini kilichomtia nguvu Musa kuwaongoza Waisraeli?
3 Roho takatifu iliwatia nguvu wawakilishi wa Mungu. Mfikirie  Musa, ambaye aliagizwa awaongoze Waisraeli. Ni nini kilichomsaidia kushughulikia mgawo huo mzito? Yehova “[alitia] ndani yake roho Yake takatifu.” (Soma Isaya 63:11-14.) Kwa kumtia nguvu Musa kupitia roho yake takatifu, Yehova aliendelea kuwaongoza watu Wake.
4. Waisraeli wangetambuaje kwamba Musa alikuwa na roho ya Mungu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)
4 Kwa kuwa roho takatifu ni nguvu isiyoonekana, Waisraeli wangetambuaje kwamba inatenda ndani ya Musa? Roho takatifu ilimwezesha Musa kufanya miujiza na kumtangazia Farao jina la Mungu. (Kut. 7:1-3) Pia, ilimwezesha Musa kuwa na sifa nzuri kama vile upendo, upole, na subira, nazo zilimwezesha kuwaongoza Waisraeli. Alitofautiana sana na viongozi wa nchi nyingine waliokuwa wakali na wenye ubinafsi! (Kut. 5:2, 6-9) Uthibitisho ulionyesha hivi waziwazi: Yehova alikuwa amemchagua Musa awaongoze watu Wake.
5. Eleza jinsi Yehova alivyowatia nguvu wanaume wengine kati ya Waisraeli waongoze watu wake.
5 Baadaye, roho takatifu iliwatia nguvu wanaume wengine walioteuliwa na Yehova kuwaongoza watu wake. “Yoshua mwana wa Nuni alikuwa amejaa roho ya hekima.” (Kum. 34:9) “Roho ya Yehova [ilimfunika] Gideoni.” (Amu. 6:34) Na “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi.” (1 Sam. 16:13) Wanaume hao wote walitegemea roho ya Mungu iwasaidie, nayo iliwatia nguvu kutimiza mambo ambayo hawangeweza kutimiza kwa nguvu zao wenyewe. (Yos. 11:16, 17; Amu. 7:7, 22; 1 Sam. 17:37, 50) Kwa sababu hiyo, Yehova alipokea sifa anazostahili kwa matendo hayo yenye nguvu.
6. Kwa nini Mungu alitaka watu wake wawaheshimu wanaume walioongoza katika Israeli?
6 Waisraeli walipaswa kutendaje walipoona uthibitisho ulio wazi kwamba wanaume hao walikuwa wametiwa nguvu na roho takatifu? Watu waliponung’unika kuhusu uongozi wa Musa, Yehova aliuliza hivi: “Watu hawa wataendelea kunitendea bila heshima mpaka wakati gani?” (Hes. 14:2, 11) Kwa hakika, Yehova aliwachagua Musa, Yoshua, Gideoni, na Daudi wamwakilishe akiwa Kiongozi wao. Watu walipowatii wanaume hao, kihalisi walikuwa wakimtii Yehova akiwa Kiongozi wao.
WALISAIDIWA NA MALAIKA
7. Malaika walimsaidiaje Musa?
7 Malaika waliwasaidia wawakilishi wa Mungu. (Soma Waebrania 1:7, 14.) Yehova alitumia malaika kumpa mgawo, kumzoeza, na kumwelekeza Musa. Mungu alimtuma Musa “akiwa mtawala na pia mkombozi kwa mkono wa malaika aliyemtokea katika mti wa miiba.” (Mdo. 7:35) Sheria ambayo Musa alitumia kuwaongoza Waisraeli ilitoka kwa Yehova, nayo “ilipitishwa kupitia malaika.” (Gal. 3:19) Na Yehova akamwambia hivi: “Waongoze watu kwenda mahali nilipokuambia juu yake. Tazama! Malaika wangu ataenda mbele yako.” (Kut. 32:34) Biblia haisemi kwamba Waisraeli waliona malaika aliyejivika mwili wa kibinadamu akifanya mambo hayo. Hata hivyo, jinsi Musa alivyowaagiza na kuwaongoza watu kulithibitisha kwamba alisaidiwa na uwezo unaozidi wa kibinadamu.
8. Malaika waliwasaidiaje Yoshua na Hezekia?
8 Yoshua ambaye alimrithi Musa, alitiwa nguvu na “mkuu wa jeshi la Yehova” kuwaongoza watu wa Mungu walipopigana na Wakanaani; nao Waisraeli wakashinda. (Yos. 5:13-15; 6:2, 21) Baadaye, Mfalme Hezekia alikabiliana na jeshi kubwa sana la Ashuru ambalo lilitishia kuvamia Yerusalemu. Katika usiku mmoja, “malaika wa Yehova alitoka, akapiga na kuwaua watu 185,000.”—2 Fal. 19:35.
9. Je, kutokamilika kwa wawakilishi wa Mungu kuliwapa Waisraeli sababu ya kukataa mwongozo wao? Eleza.
 9 Ingawa malaika walikuwa wakamilifu, wanaume waliokuwa wakisaidiwa hawakuwa wakamilifu. Pindi fulani Musa alikosa kulitakasa jina la Yehova. (Hes. 20:12) Yoshua alipuuza kutafuta mwongozo wa Mungu kabla ya kufanya agano pamoja na Wagibeoni. (Yos. 9:14, 15) Na kwa kipindi kifupi, “moyo [wa Hezekia] ulikuwa wenye majivuno.” (2 Nya. 32:25, 26) Hata hivyo, licha ya kutokamilika kwa wanaume hao, Waisraeli walitarajiwa kufuata mwongozo wao. Yehova alikuwa akiwategemeza wanaume hao kupitia wawakilishi wake wenye uwezo unaopita wa kibinadamu. Naam, Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake.
WALIONGOZWA NA NENO LA MUNGU
10. Musa aliongozwaje na Sheria ya Mungu?
10 Neno la Mungu liliwaongoza wawakilishi wake. Biblia inarejelea Sheria waliyopewa Waisraeli kuwa “sheria ya Musa.” (1 Fal. 2:3) Hata hivyo, Maandiko yanasema kuwa Yehova ndiye Mpaji-Sheria, na Musa alikuwa chini ya Sheria hiyo. (2 Nya. 34:14) Baada ya Yehova kutoa maagizo ya jinsi atakavyojenga maskani, “Musa akafanya kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.”—Kut. 40:1-16.
11, 12. (a) Yoshua na wafalme ambao waliwaongoza watu wa Mungu walipaswa kufanya nini? (b) Neno la Mungu lilikuwa na matokeo gani kwa wanaume walioongoza watu wa Mungu?
11 Tangu mwanzo wa uongozi wake, Yoshua alikuwa na nakala ya Neno la Mungu. Aliambiwa hivi: “Nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake.” (Yos. 1:8) Baadaye, wafalme waliowatawala watu wa Mungu walifanya vivyo hivyo. Walipaswa kusoma Sheria hiyo kila siku, kujiandikia nakala, na “kushika maneno yote ya sheria hii na masharti haya kwa kuyafanya.”—Soma Kumbukumbu la Torati 17:18-20.
12 Neno la Mungu lilikuwa na matokeo gani kwa wanaume walioongoza? Fikiria mfano wa Mfalme Yosia. Hati iliyokuwa na Sheria ya Musa ilipopatikana, mwandishi wa Yosia alimsomea. * Mfalme alitendaje? “Mara tu mfalme alipoyasikia maneno ya kile kitabu cha ile sheria, akayararua mavazi yake mara moja.” Lakini alifanya mengi zaidi. Akiongozwa na Neno la Mungu, Yosia alianza kampeni kubwa dhidi ya ibada ya sanamu na kupanga kuwe na sherehe kubwa ya Pasaka ambayo haikuwahi kufanywa kabla ya hapo. (2 Fal. 22:11; 23:1-23) Kwa kuwa waliongozwa na Neno la Mungu, Yosia na viongozi wengine waaminifu walikuwa tayari kubadili na kufafanua mwongozo waliowapa watu wa Mungu. Mabadiliko hayo yaliwapatanisha watu wa kale wa Mungu na mapenzi yake.
13. Kulikuwa na tofauti gani kati ya viongozi wa watu wa Mungu na wa mataifa ya kipagani?
13 Wafalme hao waaminifu walitofautiana sana na viongozi wa mataifa mengine ambao waliongozwa na hekima ya kibinadamu na kufanya mipango bila kuzingatia wakati ujao! Chini ya uongozi wa Wakanaani, watu walifanya mambo yenye kuchukiza yaliyotia ndani ngono kati ya watu wa familia, ngono kati ya watu wa jinsia moja, ngono na wanyama, kudhabihu watoto, na ibada ya sanamu yenye kuchukiza. (Law. 18:6, 21-25) Isitoshe, viongozi wa Babiloni na wa Misri hawakufuata njia zilizothibitishwa kisayansi kuhusu kanuni za usafi ambazo Mungu aliwapa Waisraeli. (Hes. 19:13) Tofauti nao, watu wa kale wa Mungu waliona jinsi viongozi wao waaminifu walivyoendeleza  usafi wa kiroho, kiadili, na kimwili. Ni wazi kwamba Yehova alikuwa akiwaongoza.
14. Kwa nini Yehova aliwatia nidhamu baadhi ya viongozi wa watu wake?
14 Si wafalme wote waliowatawala watu wa kale wa Mungu waliofuata maagizo yake. Wafalme ambao hawakumtii Yehova walikataa mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, malaika zake, na Neno lake. Katika visa fulani, Yehova aliwatia nidhamu au kuwaondoa viongozi hao. (1 Sam. 13:13, 14) Kwa wakati uliofaa, angemchagua mtu mwenye uwezo wa hali ya juu kuliko mwanadamu yeyote aliyekuwa amemtumia kabla ya hapo.
YEHOVA AMTEUA KIONGOZI MKAMILIFU
15. (a) Manabii walionyeshaje kwamba kungekuwa na kiongozi wa pekee? (b) Kiongozi aliyetabiriwa alikuwa nani?
15 Kwa karne nyingi, Yehova alitabiri kwamba angeteua kiongozi anayestahili kwa njia ya pekee kuwaongoza watu wake. Musa aliwaambia hivi Waisraeli: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kum. 18:15) Isaya alitabiri kwamba Huyo angekuwa “kiongozi na kamanda.” (Isa. 55:4) Na Danieli aliongozwa na roho kuandika kuhusu kuja kwa “Masihi aliye Kiongozi.” (Dan. 9:25) Mwishowe, Yesu Kristo alijitambulisha kuwa “Kiongozi” wa watu wa Mungu. (Soma Mathayo 23:10.) Wanafunzi wa Yesu walimfuata kwa hiari, nao walikiri kwamba alikuwa amechaguliwa na Yehova. (Yoh. 6:68, 69) Ni nini kilichowasadikisha kwamba Yehova alikuwa akimtumia Yesu Kristo kuongoza watu wake?
16. Ni nini kilichothibitisha kwamba Yesu alikuwa ametiwa nguvu na roho takatifu?
16 Roho takatifu ilimtia nguvu Yesu. Yesu alipobatizwa, Yohana Mbatizaji aliona “mbingu zikifunguka, na roho ikashuka juu yake kama njiwa.” Baadaye, “roho ikamshurutisha aende nyikani.” (Marko 1:10-12) Kwa muda wote wa huduma yake hapa duniani, Yesu alitiwa nguvu na roho takatifu ya Mungu kufanya miujiza na kuzungumza kwa mamlaka iliyotoka kwa Mungu. (Mdo. 10:38) Kwa kuongezea, roho takatifu ilimsaidia Yesu kusitawisha kikamili sifa za tunda la roho kutia ndani upendo, shangwe, na imani thabiti. (Yoh. 15:9; Ebr. 12:2) Hakuna kiongozi mwingine aliyeonyesha sifa kama hizo. Yehova alijua kuwa Yesu ndiye kiongozi anayefaa.
Malaika wamtokea Yesu na kumtia nguvu
Malaika walimsaidiaje Yesu muda mfupi baada ya kubatizwa? (Tazama fungu la 17)
17. Malaika walifanya nini ili kumsaidia Yesu?
17 Malaika walimsaidia Yesu. Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, “malaika wakaja na kuanza kumhudumia.” (Mt. 4:11) Saa kadhaa kabla ya kifo chake, “malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Yesu alikuwa na uhakika  kwamba Yehova angetuma malaika wakati wowote alipohitaji msaada ili kutimiza mapenzi ya Mungu.—Mt. 26:53.
18, 19. Neno la Mungu liliongozaje maisha na mafundisho ya Yesu?
18 Neno la Mungu lilimwongoza Yesu. Tangu mwanzo wa huduma yake, Yesu aliruhusu Maandiko yamwongoze. (Mt. 4:4) Kwa kweli, alikuwa tayari kutii Neno la Mungu hadi kufikia kifo juu ya mti wa mateso. Hata maneno yake ya mwisho kabla ya kufa yalitia ndani manukuu ya unabii unaomhusu Masihi. (Mt. 27:46; Luka 23:46) Tofauti naye, viongozi wa kidini wa wakati huo walipuuza Neno la Mungu kila mara lilipopingana na desturi zao. Akinukuu maneno ya Yehova yaliyo katika unabii wa Isaya, Yesu alisema hivi kuwahusu: “Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, bali moyo wao umepelekwa mbali nami. Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.” (Mt. 15:7-9) Je, kweli Yehova angemchagua yeyote kati ya wanaume hao aongoze watu wake?
19 Yesu hakuruhusu Neno la Mungu liongoze matendo yake tu, bali pia mambo aliyofundisha. Alipoulizwa kuhusu mambo ya kidini ambayo watu walibishania, hakurejelea hekima yake nyingi au uzoefu wake usio na kifani. Badala yake, alitegemea kikamili hekima ya Maandiko. (Mt. 22:33-40) Na badala ya kuwatumbuiza wasikilizaji wake na hadithi kuhusu maisha yake akiwa mbinguni au uumbaji wa ulimwengu, “[alifungua] akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.” (Luka 24:32, 45) Yesu alilipenda Neno la Mungu, na alitamani kulishiriki pamoja na wengine.
20. (a) Yesu alionyeshaje kwamba alijitiisha kwa Mungu? (b) Tofauti kati ya Yesu na Herode Agripa wa Kwanza inatufundisha nini kuhusu kiongozi anayechaguliwa na Yehova?
20 Ijapokuwa Yesu aliwashangaza wasikilizaji wake kwa “maneno yenye kuvutia sana,” alimpa sifa Mwalimu wake, Yehova. (Luka 4:22) Mwanamume fulani tajiri alipojaribu kumtukuza Yesu kwa kumwita “Mwalimu Mwema,” Yesu alionyesha sifa ya kiasi kwa kumjibu hivi: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Marko 10:17, 18) Alitofautiana sana na Herode Agripa wa Kwanza, ambaye alikuwa mfalme, au kiongozi wa Yudea miaka minane hivi baadaye! Katika mkutano wa mashauriano, Herode alijivika “vazi la kifalme.” Umati uliokuwa ukimsifu ulipaaza sauti hivi: “Ni sauti ya mungu, wala si ya mwanadamu!” Inaelekea Herode alifurahi aliposifiwa. Ni nini kilichotukia muda mfupi baadaye? “Papo hapo malaika wa Yehova akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; naye akaliwa na wadudu akakata pumzi.” (Mdo. 12:21-23) Kwa hakika, mtazamaji mwenye usawaziko angeweza kukata kauli kwamba Herode hakuwa kiongozi aliyechaguliwa na Yehova. Kwa upande mwingine, Yesu alionyesha uthibitisho wenye kusadikisha kwamba alikuwa amechaguliwa na Mungu, na sikuzote alimtukuza Yehova akiwa Kiongozi Mkuu wa watu wake.
21. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
21 Uongozi wa Yesu haukukusudiwa uwe wa miaka michache tu. Baada ya kufufuliwa, alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. . . Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:18-20) Lakini akiwa roho asiyeonekana mbinguni, Yesu angewaongozaje watu wa Mungu duniani? Yehova angetumia nani kufanya kazi chini ya uongozi wa Kristo na kuwaongoza watu Wake? Na Wakristo wangewezaje kutambua wawakilishi wake? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FAIDA YA KUJAA ROHO MTAKATIFU

NGUVU NA FAIDA ZA MSAMAHA

🔰 MBINU ZA KUFUNGA NA KUOMBA 🛐*